1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zaidi ya watu 63,000 wamepotea au kutoweka kwa uhamiaji

26 Machi 2024

Shirika la Uhamiaji Duniani IOM limetoa ripoti ya utafiti uliobanisha kuwa zaidi ya watu 63,000 wamepotea ama kutoweka kwa uhamiaji duniani kwa kipindi cha muongo mmoja huku vifo vingi vikitokana na kuzama majini

https://p.dw.com/p/4e9L3
 Internationaler Flüchtlingsorganisation IOM Logo
Shirika la Uhamiaji Duniani IOM limesema kuwa wahamiaji wengi hupoteza maisha bahariniPicha: Jakub Porzycki/NurPhoto/picture alliance

   

Shirika la Uhamiaji Duniani IOM limetoa ripoti ya utafiti uliobanishwa kuwa zaidi ya watu 63,000 wamepotea ama kutoweka kwenye njia za uhamiaji kote ulimwenguni kati ya mwaka 2014 na mwaka 2023, Vifo vingi vikitajwa kuwa ni kutokana na kuzama majini.

Ripoti iliyochapishwa na Shirika hilo la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) kwenye Mradi wake wa wahamiaji waliopotea imeonyesha kuwa vifo vya zaidi watu 28,000 vilitokea katika bahari ya Mediterranea, ikifuatiwa na mabara ya Afrika na Asia.

Soma zaidi. UN: Kuzama baharini ndio chanzo kikuu cha vifo vya wahamiaji

Karibu 60% ya vifo vilivyorekodiwa vilihusishwa na kuzama, na zaidi ya theluthi moja ya waliotambuliwa walitoka nchi zilizoko kwenye migogoro, ikiwa ni pamoja na Afghanistan, Myanmar, Syria na Ethiopia.

Takwimu za IOM zimeonyesha kuwa mwaka 2023 ndio ulikuwa mwaka mbaya zaidi kwa wahamiaji katika kipindi cha muongo mmoja uliopita, vifo vya watu 8,541 vimetokana kwa sehemu kubwa na kuzama kwenye maji katika bahari ya Mediterania.

Libyen I Rettung von Migranten im zentralen Mittelmeer
Boti ya waokoaji wa uhamiaji katika bahari ya MeditaraniaPicha: Simone Boccaccio/SOPA/IMAGO

Ripoti hiyo inasema ongezeko hilo la vifo huenda linahusishwa na ongezeko la watu kuondoka katika nchi zao na, vivyo hivyo, kuanguka kwa meli.

Soma zaidi. Wahamiaji 600 waingia kisiwa cha Italia cha Lampedusa

Mfano katika pwani ya Tunisia, ripoti hiyo inasema takribani watu 729 walikufa  nje ya pwani hiyo mwaka 2023 tofauti na idadi ya watu 462 waliokufa kwa mwaka wa nyuma yake wa 2022.


Msemaji wa taasisi ya takwimu ya IOM Jorge Galindo amesema "Takwimu zinatisha sana. Tumeona miaka kumi na kuendelea,  watu wanaendelea kupoteza maisha wakitafuta maisha bora. Tuliona kwa mfano mwaka 2023 ndio mwaka wa vifo zaidi kuwahi kuripotiwa kwa vifo zaidi ya 8500. Na sababu ni Idadi kubwa ya watu, zaidi ya 60% ya vifo vilivyorekodiwa na mradi vilitokana na kufa maji. Katika Bahari ya Mediterania pekee, tunaona, zaidi ya vifo 28,000 na kupotea vimerekodiwa."

EU yaahidi kutoa mabilioni ya fedha 

Kwa upande mwingine, vyama vinavyopinga uhamiaji vikiwa vikiendelea kupata ushawishi kote barani ulaya, serikali zimejaribu kuzuia uhamiaji kuingia katika nchi zao kwa kuahidi fedha kwa nchi za Mediterania kama vile Tunisia na Misri ili kuudhibiti uhamiaji.

Libya
Wahamijai waliotoka nchini Libya wakiwa katikati mwa bahari ya Mediterania kuelekea barani UlayaPicha: Simone Boccaccio/SOPA/IMAGO

Mapema mwezi huu, Umoja wa Ulaya uliahidi mfuko wa ufadhili wa euro bilioni 7.4 kwa Misri, mpango ambao Waziri Mkuu wa Italia Giorgia Meloni alielezea kama njia bora ya kushughulikia mtiririko wa wahamaji."

Soma zaidi. Uingereza ingali na lengo kuwapeleka wakimbizi Rwanda

Akiongezea wakati wa kuwasilisha ripoti ya Shirika IOM, Jorge Galindo amesema "Nadhani ni muhimu sana kuhakikisha kuwa kuna takwimu, kurekodi vifo hivi, lakini pia takwimu hizi ni vitambulisho. Na serikali zinapaswa kushirikiana na mashirika ya kiraia kuhakikisha kuwa familia ambazo zimeachwa, bila kujua waliko wapendwa wao. wanaweza kupata ufikiaji bora wa mabaki ya watu waliokufa. Na hiyo itawaletea hali ya kufungwa."

Hata hivyo wakati serikali za nchi kadhaa za Ulaya, zikiwemo Italia, Hungary na Uingereza zikiweka kipaumbele cha kuzuia uhamiaji, viongozi wa dini ikiwemo Papa Fransis wamekuwa wakitoa wito kwa kuwaonea huruma wahamiaji kama namna ya kujibu kile mataifa ya ulaya yaavyofanya kuwadhibiti wahamiaji wanaovuka kupitiia bahari ya meditreania.

.