1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

APEC kuzingatia zaidi masuala ya mazingira na usawa

Angela Mdungu
14 Novemba 2023

Waziri wa fedha wa Marekani Janeth Yellen amesema kuwa viongozi wa mataifa ya jumuiya ya uchumi ya Asia na Pasifiki wanataka kuboresha ushirikiano kwa kuangazia masuala kama vile ukosefu wa usawa na kulinda mazingira.

https://p.dw.com/p/4Ymc4
Marais Xi Jinping na Joe Biden walipokutana 2022
Marais Xi Jinping na Joe Biden walipokutana 2022Picha: Saul Loeb/AFP/Getty Images

Yellen ameyasema hayo katika mkutano na waandishi wa habari mwishoni mwa mkutano uliowajumuisha mawaziri wa fedha wa Jumuiya ya uchumi ya Asia na Pasifiki APEC unaofanyika mjini San Francisco, Marekani.

Ameyasema hayo akitolea mfano sheria ya kupunguza mfumuko wa bei ambayo ni moja ya mafanikio makubwa na muhimu ya rais wa Marekani Joe Biden.

Yellen amesema kuwa wanahitaji kukuza zaidi hali ya uchumi kwa kuongeza upatikanaji wa nguvu kazi, uvumbuzi na uwekezaji katika miundombinu katika njia ambazo ni endelevu na zinazopunguza kutokuwepo kwa usawa. 

Soma zaidi: Beijing yashinikiza maelewano zaidi na Marekani kabla ya mkutano wa Xi na Biden

Hayo yanajiri wakati Utawala wa rais Joe Biden, jana jumatatu uliashiria kuwa utaahirisha rasimu ya makubaliano  na bara la Asia iliyopangwa kuwasilishwa kwatika mkutano huo wa kilele wa  Jumuiya ya uchumi ya Asia na Pasifiki baada ya kukosolewa vikali ndani ya Marekani.

Bado kazi kubwa inahitajika kuboresha kipengele cha biashara

Akizungumzia mkataba huo, Waziri wa Fedha wa Marekani Janet Yellen amesema kuwa bado kuna kazi inayohitajika kufanywa katika sehemu ya kipengele cha biashara cha kile kinachoitwa mfumo  wa mafanikio wa Jumuiya ya kiuchumi ya Indo Pasifiki.  Licha ya hayo, Yellen alibainisha kuwa juhudi za kujenga uhusiano imara na China zina mwelekeo mzuri. 

Waziri wa fedha wa Marekani Janet Yellen
Waziri wa fedha wa Marekani Janet YellenPicha: SAM PANTHAKY/AFP

Hayo yanajiri wakati China inafanya juhudi za kuimarisha uhusiano wake na Marekani katika mkutano uliosubiriwa kwa muda mrefu kati ya Marais wa mataifa hayo wiki hii.

Katika mkutano huo, Rais Biden ni mwenyeji wa mataifa 20 wanachama wa jumuiya. Anatarajiwa kukutana na Rais wa China Xi Jin Ping mjini Carlifonia kando ya majadiliano ya  mkutano huo wa kilele. Marais hao wa China na Marekani watakutana kwa mara ya kwanza baada ya mwaka mmoja licha ya mivutano ya kibiashara, vikwazo na mzozo kuhusu Taiwan.