1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali: Kimbunga Hidaya sio kitisho tena kwa Tanzania.

Saumu Mwasimba
5 Mei 2024

Kimbunga Hidaya kimepiga zaidi katika kisiwa cha Mafia nchini Tanzania,Jumamosi na kuleta mvua kubwa na upepo mkali.

https://p.dw.com/p/4fWCP
Kimbunga Malawi na Msumbiji
Kimbunga Freddy kilichopiga Malawi march mwaka 2023Picha: NASA/AP Photo/picture alliance

Serikali ya Tanzania imesema kimbunga hidaya kilichopiga katika pwani ya Afrika Mashariki kimeshapoteza nguvu na sio kitisho tena kwa nchi hiyo.

Hata hivyo maafisa wameutaka umma kuendelea kuwa na tahadhari kwasababu kimbunga hicho kimesababisha mvua kubwa na upepo mkali,hali itakayoendelea siku nzima ya Jumapili. 

Maeneo mengi ya Tanzania Jumamosi yalikosa umeme huku mvua kubwa ikinyesha na upepo mkali ukivuma kufuatia kimbunga Hidaya.

Kimbunga hicho kilisababisha mvua kubwa na upepo mkali nchini Tanzania na Kenya ambako kimekuwa kikishuhudiwa wakati mataifa hayo mawili yakikumbwa na mvua kubwa za masika na mafuriko ambayo yamesababisha vifo vya watu 400 katika eneo zima la Afrika Mashariki ndani ya kipindi cha wiki za hivi karibuni.

Mto uliofurika mtaa wa Mathare Nairobi
Mafuriko KenyaPicha: IMAGO/Xinhua

Mamlaka ya hali ya hewa ya Tanzania imechapisha taarifa kwenye ukurasa wa X  leo Jumapili inayosema kimbunga Hidaya kimeshadhoofika kabisa baada ya kupiga kisiwa cha Mafia katika bahari ya hindi siku ya  Jumamosi.

Taarifa hiyo pia imeeleza kwamba sasa hakuna tena kitisho cha kimbunga hicho ndani ya Tanzania.

Taarifa za kimbunga Hidaya kilisababisha maeneo ya fukwe za bahari ya Hindi kukimbiwa na maduka kufungwa pamoja na shughuli za usafiri wa baharini kusitishwa katika visiwa vya Zanzibar.Soma pia: Umeme wakatika Tanzania wakati Kimbunga Hidaya kikikaribia

Wakati kimbunga hicho kikikaribia kupiga, mvua kubwa zilinyesha kuliko kawaida katika maeneo ya pwani ingawa hakuna ripoti za wahanga au kutokea  uharibifu.

Nchini Tanzania Takriban watu 155 wamepoteza maisha kufuatia athari za mvua kubwa zinazohusishwa na hali ya hewa ya ElNino,ikiwemo mafuriko na maporomoko ya ardhi mwezi uliopita wa Aprili.

Katika nchi jirani ya Kenya ambako pia tahadhari zilichukuliwa kufuatia kimbunga Hidaya, jumla ya watu 210 mpaka sasa wamepoteza maisha katika matukio yanayohusishwa na mafuriko.