1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSomalia

Somalia yajadiliwa kujiunga na jumuiya ya Afrika Mashariki

31 Agosti 2023

Azma ya Somalia kujiunga na jumuiya ya Afrika Mashariki imefikia hatua muhimu baada ya majadiliano kuhitimishwa.Somalia iliwasilisha kwa mara ya kwanza miaka 11 iliyopita ombi la kutaka kujiunga na EAC.

https://p.dw.com/p/4Vohn
Somalia Präsident Hassan Sheikh Mohamud
Rais wa Somalia Hassan Sheikh MohamudPicha: Farah Abdi Warsameh/AP/picture alliance

Vita na serikali iliyotatizwa na wanamgambo ndiyo mambo yaliyokwamisha juhudi hizo.

Hata hivyo mambo yamebadilika na sasa Somalia imestawi kupitia harakati za pamoja za kikanda.

Wataalam na wadau wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wanajiandaakuwasilisha ripoti maalum kwa baraza la mawaziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Baraza hilo lina wajibu wa kuitathmini na hatimaye kutoa mapendekezo kwa viongozi wa ngazi ya juu ambao ni marais wa Jumuiya hiyo kabla ya Somalia kujiunga.

Soma pia:Somalia yazipiga marufuku TikTok, Telegram na 1XBet

Duru zinaashiria kuwa huenda Somalia ikawa mwanachama mpya ifikapo Novemba iwapo kasi ya mchakato itaongezwa.

Daud Aweiss ni waziri wa habari na utamaduni nchini Somalia amesema tayari wamekamilisha taratibu muhimu za kujiunga.

"Somalia itakuwa mshirika muhimu hasa katika masuala ya usalama na uchumi." Alisema

Aliongeza kwamba Somalia ina subiri kwa hamu kujiunga katika jumuiya hiyo ya Afrika mashariki, ambayo imezidi kupanua ushawishi wake kwa mataifa ya kusini mwa Afrika.

Mazungumzo hayo yanatoa nuru kwa Somalia?

Mazungumzo hayo ya siku 10 yalianza mapema wiki iliyopita kwenye ukumbi wa taasisi ya elimu ya uongozi iliyoko eneo la Lower Kabete.

Kwenye ufunguzi wa Kikao, waziri wa masuala ya Afrika Mashariki wa Kenya, Rebecca Miano alibainisha kuwa jumuiya ya EAC inapania kuupanua wigo wake ili kuimarisha biashara kati ya nchi wanachama na jumuiya nyengine.

Kikao cha 22 cha jumuiya ya Afrika mashariki ndicho kilichoridhia hatua ya kuanza majadiliano ya kuinga Somalia na EAC.

Kwanini Al-Shabab inawatia hofu wasomali?

Soma pia:Somalia yasema imewaua wapiganaji 40 wa Al Shaabab

Kuhusu suala la usalama, Itakumbukwa kuwa tayari  vikosi vya nchi wanachama vinaisaidia serikali ya Somalia kudumisha usalama na kuiwezesha kuilinda mipaka yao kupitia kikosi cha ATMIS kilichorithi majukumu ya AMISOM.

Kwa upande wake, Somalia imeahidi kuwa Itakuwa mshirika muhimu na wa manufaa kwa jumuiya ya Afrika mashariki.

Vipi Somalia itachangia katika jumuiya?

Somalia imebainisha kuwa uanachama wake utaimarisha nguvu Zake kupambana na changamoto za usalama zinazolizonga eneo la pembe ya Afrika.

Uganda Dr. Peter Mathuki
Katibu mkuu wa jumuiya ya Afrika mashariki Dr Peter MathukiPicha: Emmanuel Lubega/DW

Kadhalika hatua hiyoitalipanua soko la bidhaa zakena biashara na nchi wanachama.

Kulingana na wawakilishi waliokuwa kikaoni ,Somalia inajivunia nguvu kazi kubwa ya vijana, utajiri mkubwa wa mali asili na kilimo.

Ili kulisisitizia hilo, katibu mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Dr Peter Mathuki anasema kuwa uanachama wa Somalia utaipa fursa ya kufaidika na miradi ya miundo mbinu kama vile usafiri, biashara na utangamano.

Somalia ndiyo nchi iliyo na ukanda mrefu zaidi wa kilomita alfu 3 wa pwani unaoliunganisha bara la Afrika na rasi ya Arabuni.

Soma pia:Kenya: Mashambulizi yachangia mpaka na Somalia kutofunguliwa

Ombi la kwanza la kujiunga na jumuiya ya Afrika Mashariki liliwasilishwa mwaka 2012 ila halikupata ridhaa kwa sababu kadha wa kadha.

 Kwa upande mwengine, jumuiya ya Afrika Mashariki imekosolewa kwa kuiunga Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo ambayo bado eneo lake la mashariki linazongwa na vita kwa kiasi ya miongo miwili sasa.

Hata hivyo, Burundi  na Sudan Kusini ambazo zilijiunga kabla ya DRC, bado hazijaweza kuchangia kikamilifu kwenye bajeti ya Jumuiya na kuziachia mzigo huo Kenya, Uganda na Tanzania kwa kiasi kikubwa inaeleza ripoti ya tathmini ya mwaka 2020/21 ya bunge la Afrika Mashariki