1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Somalia yaitisha mkutano wa kimataifa juu ya Al-Shabaab

John Juma
1 Februari 2023

Rais Hassan Sheikh Mohamud wa Somalia anatarajiwa kuwa mwenyeji wa mkutano wa kilele wa kikanda utakaojadili mapambano dhidi ya kundi la kigaidi la Al-Shabaab lenye mafungamano na kundi lijiitalo Dola la Kiislamu.

https://p.dw.com/p/4MxwN
Somalia Hassan Sheikh Mohamud
Picha: Feisal Omar/REUTERS

Viongozi kutoka katika mataifa yenye wanajeshi wake kwenye Kikosi cha Mpito cha Umoja wa Afrika nchini Somalia (ATMIS) kinachohusika na operesheni dhidi ya wanamgambo, watajadili njia za kupambana na mashambulizi yanayofanywa na Al-Shabaab. 

Wizara ya habari ya Somalia imesema ulinzi mkali umeimarishwa kwenye mji mkuu Mogadishu tangu jana, ambako mawaziri wa ulinzi kutoka Djibouti, Ethiopia na Kenya wamekuwa wakiandaa mkutano huo wa siku mbili. 

Ingawa wapiganaji wa Al-Shabaab walifurushwa kutoka Mogadishu na majeshi ya Umoja wa Afrika mwaka 2011, bado wanadhibiti baadhi ya maeneo ya nchi hiyo na wamefanya mashambulizi kadhaa ndani ya Somalia na kwenye nchi jirani.