1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa zamani wa Tanzania afariki dunia akiwa na miaka 98

1 Machi 2024

Rais wa zamani wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi, aliyeanzisha mfumo wa demokrasia ya vyama vingi katika taifa hilo la Afrika Mashariki, amefariki dunia jana akiwa na umri wa miaka 98.

https://p.dw.com/p/4d3Ux
Ali Hassan Mwinyi
Rais wa zamani wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi.Picha: AFP/Getty Images

Tangazo la kifo cha rais huyo mstaafu lilitolewa na rais wa nchi hiyo, Samia Suluhu Hassan, katika ujumbe uliorushwa moja kwa moja katika televisheni ya taifa hilo, TBC.

Rais Samia alisema Mwinyi, ambaye alihudumu kwa mihula miwili kama rais wa Tanzania kutoka 1985 hadi 1995 na kabla ya hapo kama rais wa mpito wa Zanzibar kutoka 1984 hadi 1985, alifariki kutokana na saratani ya mapafu.

Soma zaidi: Mfahamu Rais ajaye wa Tanzania Samia Suluhu Hassan

Mwezi Novemba alilazwa katika hospitali moja mjini London ila baadaye akarudi Dar es Salaam kuendelea na matibabu.

Maombolezo ya siku saba

Mwinyi, Nyerere na Wakil
Kutoka kulia, aliyekuwa rais wa kwanza wa Tanzania, Julius Nyerere, mfuatizi wake, Ali Hassan Mwinyi, na aliyekuwa rais wa Zanzibar baada ya Mwinyi, Idriss AbdulwakilPicha: AFP/Getty Images

Tanzania sasa ina siku saba za maombolezo ya kifo cha Mwinyi huku bendera zikipepea nusu mlingoti, alisema Rais Samia, akiongeza kuwa kiongozi huyo aliyeleta mabadiliko ya kidemokrasia angelizikwa siku ya Jumamosi (Machi 2).

Rais William Ruto wa Kenya aliandika ujumbe wa rambirambi kwenye mtandao wa kijamii wa X, akimtaja mwendazake kama "kiongozi mkubwa ambaye alama yake haitosahaulika."

Soma zaidi: Magufuli alihutubia bunge

Mwinyi alichaguliwa na mwanzilishi wa taifa la Tanzania, Julius Kambarage Nyerere, kama mrithi wake, akichukuwa uongozi wa nchi iliyokuwa katika mgogoro mkubwa wa kiuchumi, kufuatia kushindwa kwa jaribio la Nyerere kujenga uchumi wa kisoshaliti.