1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaCameroon

Washindi wa tuzo ya Ujerumani kwa Afrika kutunukiwa Berlin

Tatu Karema
7 Juni 2023

Muungano wa Kwanza wa Kitaifa wa Amani nchini Cameroon unaowakilisha mashirika 80 wanachama, utapokea tuzo ya Ujerumani kwa Afrika mjini Berlin wakati wa msimu wa vuli.

https://p.dw.com/p/4SI8H
Deutschland | Verleihung Deutscher Afrika Preis in Berlin | Olaf Scholz mit Sikhulile Moyo
Kansela Olaf Scholz (kushoto) na mshindi wa tuzo ya Ujerumani kwa Afrika Sikhulile MoyoPicha: Michael Sohn/AP Photo/picture alliance

Katibu mkuu wa wakfu wa Ujerumani kwa Afrika unaoandaa tuzo hiyo ya kila mwaka Sabine Odhiambo, amesema jopo la uamuzi limeamua kutoa tuzo hiyo kwa muungano huo kutokana na mchango wake muhimu wa kutatua migogoro katika maeneo manne tofauti nchini humo.

Odhiambo amesema kuwa muungano huo ulitunukiwa tuzo hiyo kwa kazi yake ya kuwezesha mazungumzo ya amani na mapatano na kuongeza ushiriki wa wanawake katika kutatua migogoro nchini Cameroon. Wanawake hao wametuzwa kwa kazi yao ya kujitolea katika kukuza amani.

Mchakato ulikumbwa na nyakati tofauti

Marthe Wandou, kutoka eneo la Kaskazini mwa Cameroon, ni mmoja kati ya washindi watatu wanaouwakilisha muungano huo.

Wandou ameiambia DW kwamba mchakato huo umekumbwa na changamoto nyingi lakini pia nyakati za furaha akiongeza kuwa ushindi huo ni wao wote.

Muungano wa Kwanza wa Kitaifa wa Amani ni mtandao mkubwa zaidi wa mashirika ya wanawake yanayozingatia amani 

Muungano huo wa Kwanza wa Kitaifa wa Amani ni mtandao mkubwa na mpana zaidi wa mashirika ya wanawake yanayozingatia amani nchini Cameroon.

Ulibuniwa mnamo Januari mwaka 2021 na unajumuisha makundi 80 yanayowakilisha maeneo 10 nchini Cameroon pamoja na hadi makundi 25 tofauti ya wanawake katika jamii. Esther Omam kutoka eneo la Kusini Magharibi mwa Cameroon, amesema kuwa huo ni utambuzi mkubwa kwa kazi ya wanawake wanaokuza amani.

Kamerun | Preisträger des Deutschen Afrika-Preis 2023 - Sally Mboumien
Sally Mboumien - Mshindi kutoka Kaskazini Magharibi mwa CameroonPicha: Elisabeth Asen/DW

Wanawake wameathirika vibaya na mzozo wa kiusalama katika maeneo manne kati ya 10 nchini Cameroon.

Mkusanyiko mkubwa zaidi wa muungano huo katika historia ya Cameroon, uliwaleta pamoja zaidi ya wanawake 1800 kutoka maeneo yote 10 na idara 58 zilizowajumuisha wasichana wadogo, wanawake wakubwa, wasomi, wanariadha, wanajeshi, wasanii na wanasayansi.

Wanawake hao walitoa wito wa kusitishwa mara moja kwa mapigano na kuanzishwa tena kwa mazungumzo kati ya serikali na makundi ya waliojitenga katika maeneo yanayozungumza Kiingereza nchini Cameroon, kuhusishwa kwa wanawake katika mazungumzo ya mapatano, kuimarishwa kwa hatua za upokonyaji silaha na kubuniwa kwa vituo vya kutoa msaada wa kisaikolojia na kijamii kwa wahanga wa vita katika maeneo yenye migogoro.

Muungano wa Kwanza wa Kitaifa wa Amani una manufaa makubwa

Sally Mboumien, mshindi kutoka eneo la Kaskazini Magharibi mwa Cameroon, ameiambia DW kwamba kwa pamoja, wamejenga muungano thabiti, unaosikika na wa manufaa zaidi kuliko wale wanaonufaika kutoka na mapigano.

Washindi wa mwaka jana wa tuzo hiyo ya Ujerumani kwa Afrika walikuwa Sikhulile Moyo na Tulio de Oliveira, wanasayansi wawili kutoa Afrika Kusini walioogundua aina ya kirusi cha omicron cha COVID-19 .

Wakfu wa Ujerumani kwa Afrika umedhamiria kuimarisha mahusiano kati ya Ujerumani na Afrika kwa miaka 45.

Tangu mwaka 1993, wakfu huo umetoa tuzo hiyo ya Ujerumani kwa Afrika kwa watu kutoka bara Afrika ambao wametoa mchango mkubwa katika demokrasia, amani, haki za binadamu, usanii na utamaduni, ukuaji wa uchumi, sayansi na jamii.