1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wagonjwa Kenya wateswa na mgomo wa madaktari

19 Machi 2024

Huduma za matibabu maeneo mbali mbali nchini Kenya zimevurugika kufuatia mgomo wa kitaifa wa madaktari wagonjwa wanaotafuta huduma na kutoa wito kwa serikali kupata suluhu la haraka kuutatua mgomo huo.

https://p.dw.com/p/4duW9
Kenya-Kituo cha afya
Kituo cha afya KenyaPicha: picture-alliance/dpa/C. Ehlers

Mgomo huu ambao umeathiri hospitali za umma kote nchini Kenya umeibua hali ya mahangaiko miongoni mwa wagonjwa ambao wengi wamelalamikia kukosa huduma hasaa zinazohitaji utaalamu wa madaktari kama vile upasuaji.

Madaktari Kenya wapewa siku 5 waache kugoma

Alvester Goldmea na Billy Aoko ni miongoni mwa wagonjwa waliotafuta huduma za matibabu katika hospitali ya rufaa na mafunzo ya Jaramogi Oginga Odinga inayotegemewa sana na wakaazi Magharibi mwa Kenya, wanasema kuna utofauti katika utoaji huduma za matibabu kipini hiki cha mgomo wa madaktari.

Kenya-Madaktari
Madaktari Kenya wakimuhudumia mgonjwaPicha: picture-alliance/dpa/J. Rose

Katika hospitali kuu ya Kisumu, Goldmea anasema, "Vyenye nilikuja nikiiangalia na hii ya jana iko tofauti wanakuja kidogo" naye Aoko anasema hospitali kuu ya rufaa na mafunzo ya Jaramogii Oginga Odinga," daktari hajakuja hospitalini hatujahudumiwa bado."

Mgomo huu unaendelea huku muungano wa kitaifa wa madaktari KMPDU ukishikilia kuwa wanachama wake wataendelea na mgomo huo hadi pale mahitaji yao yatakapoangaziwa mazungomzo kati ya muungano huo na wizara ya afya yakigonga mwamba licha ya kukutana na waziri Susan Nakhumicha.

Kauli ya Madaktari Kenya juu ya mgomo unaoendelea

Baadhi ya yanayoshinikiza ni kuangaziwa upya marupurupu ya madaktari walio kwenye mafunzo ya nyanjani, utekelezwaji na jumla makubaliano ya mwaka 2017 yaliyolenga kuimarisha maslahi ya madaktari ikiwemo mishahara yao anavyoelezea katibu mkuu muungano wa madaktari KMPDU Dkt. Davji Atellah, "Mgomo ungalipo, tutaishia kuchosha kurudia maana tutakuwa katika hali hii kwa muda mrefu sana, tunalenga huu kuwa mgomo wetu wa mwisho wa mwongo huu.

Wizara ya afya hata hivyo imeratibu kuwasilisha madaktari wa nyanjani katika hospitali za umma nchini kuanzia tarehe mosi mwezi Aprili ili kutimiza mojawapo ya hitaji linaloshinikizwa na muungano wa KMPDU ambao unashikilia kuwa, ahadi hii itazingatiwa tu baada ya utekelezwaji wake.

Soma pia: Madaktari wa Nairobi waanza mgomo

Wizara ya afya ya kitaifa imeahidi kuangaziwa tatizo la mgomo wa madaktari kupitia kushirikishwa kwa washikadau muhimu kwenye asasi za serikali kauli ambayo imetolewa na waziri wa afya ya kitaifa Susan Nakhumicha, "Ni mambo ambayo yanashirikisha wizara ya elimi, Baraza la magavana, huduma ya uma, tume ya uratibu mishahara ya ummaa SRC, wizara ya afya, mkuu wa huduma za umma na  tunafurahi kuyapelekwa huko."

Miongoni mwa asasi zilizochukua hatua kwa mgomo wa madaktari ni baadhi ya serikali za kaunti mfano jimbo la Kisii ambalo liliwasilisha hoja ya kupigwa marufuku madaktari jimbo hilo kushiriki mgomo mahakama ya leba ikiidhinisha ombi hilo,  serikali jimbo la Kisumu pia limetaja mgomo huo kuwa kinyume cha Sheria.