1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSomalia

Mashambulizi ya al-Shabaab yauwa watu 10 Somalia

Sudi Mnette
22 Februari 2023

Watu 10 wameuawa nchini Somalia kufuatia mashambulizi yanayodaiwa kufanywa na kundi la Al-Shabaab, ambalo limesema lilikuwa linawalenga maafisa wa jeshi na wanamgambo ambao walihusika na mashambulizi mengine dhidi yao.

https://p.dw.com/p/4Noql
Somalia Mogadischu Terror Anschlag
Picha: Feisal Omar/REUTERS

Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, mashambulizi hayo ya Jumanne yalianza kwa mripuko wa kwenye gari na kufuatiwa na makabiliano ya risasi, ambayo yalidumu kwa muda wa saa nne, ndani ya jengo ambalo inaaminika lilikuwa na wabunge kadhaa.

Baadaye wizara ya habari ya Somalia ilisema raia 10 ndio waliopoteza maisha, ingawa haijatoa ufafanuzi wa nani aliyekuwa analengwa.

Lakini imebainisha kuwa vikosi vya usalama vimewauwa pia wanamgambo wanne.

Kundi la Al-Shabaab limeongeza mashambulizi yake kutokana na kampeni iliyoanzishwa mnamo mwezi Agosti na serikali ya Rais Hassan Sheikh Mohamud, dhidi ya kundi hilo.